Si
uchochezi kusema kuwa watawala wetu wameshindwa, tena vibaya sana. Ni
aibu kwa taifa ambalo limesherehekea miaka 53 ya uhuru kushindwa kufanya
maamuzi magumu hadi lishinikizwe na wafadhili. Tishio na amri ya hivi
karibuni toka kwa serikali ya Marekani kwa Tanzania kuwa haitatoa fedha
za Changamoto za Milenia (MCC) kama serikali haitawachukulia hatua
watuhumiwa wa kashfa ya uchotaji wa mabilioni ya fedha za umma, escrow
ni somo tosha.
Heri
wafadhili wamenena. Hili ni pigo na aibu kwa rais Jakaya Kikwete,
serikali na CCM ambao wamekuwa wakiwahadaa watanzania kuwa wako
madarakani kwa maslahi yao wakati hali ni tofauti. Huu ni ushahidi kuwa
CCM na serikali yake wamewekwa mfukoni na mafisadi. Hali ikiendelea
hivi, watawala wetu wataipeleka nchi kubaya.
Huu ni ushahidi tosha kuwa utawala wa sasa umechoka, upumzishwe ili
wenye uwezo watawale na kusafisha uchafu uliopo. Inakuwaje wananchi
wanashindwa kuona haya na kuiwajibisha vilivyo CCM kwa kuishikisha
adabu?
Ni
ajabu kwa nchi inayojidai kuwa na utawala wa sheria lakini ikawekwa
mifukono mwa matapeli wachache, wasaka tonge na wahalifu wa kawaida.
Ziko wapi tambo za kupambana na biashara ya madawa ya kulevya? Nani
anawagusa? Je hawa hawana ubia kwenye serikali ya sasa? Je hawa
hawajaiweka serikali mfukoni? Asitokee mtu akaniambia kuwa hawajulikani.
Mbona rais alishakiri kupewa orodha ya wauza unga asiifanyie kazi kwa
sababu ajuazo? Je inakuwaje tunashindwa kupambana na ufisadi ilhali
tukijua kuwa ni kikwazo kwa maendeleo ya taifa? Je ni kwa vile mafisadi
ni washirika wa nyuma ya pazia ya watawala wetu?
Najua
wengi wanaweza kusema tunaizushia serikali. Kama watachunguza sababu
za serikali kuruhusu ufisadi kuwa sehemu ya maisha ya serikali yetu,
wataelewa tunachosema. Hivi kweli nchi inayoamriwa na wafadhili la
kufanya ni huru? Je kwa uzembe na upofu wetu tunapaswa kuwalaumu
wafadhili kwa kuingilia mambo yetu? Watashindwaje kuingilia iwapo
tunafanya mambo ya kitoto na ya hovyo? Imefikia mahali hata bunge
linatoa maagizo halafu wakubwa wanayadharau na kuja na mambo yasiyo
ingia kichwani kama ilivyotokea juzi wakati Ikulu iliposema kuwa
haitawawajibisha watuhumiwa wa wizi wa escrow wala kuchukua hatua hadi
ifanye uchunguzi wake. Tambo za ikulu zimeishia wapi baada ya kubanwa?
Ndani ya wiki moja ikulu, ikiwa imechanganyikiwa na kujichanganya ilitoa
tamko jingine la kijichanganya zaidi ikisema kuwa rais atawashughulikia
watuhumiwa ndani ya wiki moja. Hii maana yake ni kwamba ikulu imeminywa
na kufanya kile ambacho haikutaka kufanya. Maana ukiangalia timing ya
tamko la Marekani na mkengeuko wa Ikulu unagundua kuwa hata kama rais
atawawajibisha wahusika si kwa kutaka bali kulazimishwa na wafadhili. Je
rais au chama kinachounda serikali vya namna hii bado vinawafaa
watanzania? Je ni vibaya kusema kuwa rais amegeuka mhimili wa ufisadi
anaopaswa kuuchikia na kupamba nao? Je ni kwanini inakuwa hivi kama rais
hanufaiki na jinai hii au kuishiriki?
Ushahidi
wa kimazingira unaonyesha wazi kuwa, kama si papara za bunge, au tuseme
kuwekwa sawa na kuingia mkenge, lilipaswa kuiwajibisha serikali yote.
Kwa vile inaonyesha escrow ni dili lao. Haiwezekani mawaziri tena
waandamizi na maafisa wengi wa serikali waruhusu wizi wa mabilioni hivi
kusiwe na mkono wa wakubwa zao. Nani anakanusha kutajwa kwa afisa wa
ikulu Prosper Mbena anayedaiwa na kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali
(PAC) kuwa aliandika barua ya kushinikiza pesa zichotwe? Je hapa
tunatafuta ushahidi upi wa kuihusisha ikulu? Ushahidi mwingine ni ukimya
wa muda mrefu wa serikali. Hata kitendo cha rais kusuasua hadi
alazimishwe na wafadhili kuchukua hatua ni ushahidi tosha ukiachia mbali
rais kuhusishwa moja kwa moja na uletaji wa kampuni jizi ya IPTL hapo
mwaka 2004.
Laiti
wafadhili wangekwenda mbele zaidi na kuhakikisha hili jinni
linalotunyonya damu IPTL linafurushwa na wahusika kufungwa, wangekuwa
wametukomboa hata kama wakubwa watalalamika kuwa wanaingiliwa. Kwanini
wasiingiliwe iwapo wamejirahisi kiasi cha kuacha mafisadi wajifanyie
watakavyo? Kwanini wasiingiliwe iwapo wameonyesha wazi walivyo wa hovyo
na fisadi? Nani angeweza kumwamrisha baba wa taifa mwalimu Julius
Nyerere katika lolote? Je ilikuwaje Nyerere akaogopewa na kutopewa amri?
Jibu ni rahisi. Alikuwa msafi na mwenye visheni tofauti na hawa
walioigeuza ikulu deni la wezi kama alivyowahi kuonya Nyerere huku
akiwakataa wengi wa tunaowaona leo madarakani wakiyafuja ili kutimiza
utabiri na madai ya nguli huyu (Mungu amlaze pahali pema peponi). Rais
anayeamrishwa kufanya alichoapa kufanya amebaki na nini? Je nafsi zo
zinawasuta? Je sisi tunawasuta na kuwawajibisha au kuendelea kuwagwaya?
Tumalizie
kwa kuwataka watanzania kutorudia makosa. Kwenye uchaguzi ujao licha ya
kuhoji ni kwanini ufisadi uliachiwa kuwa sehemu ya utawala wasiangalie
sura wala ukongwe wa chama. Wahakikishe wanajipatia serikali safi, mpya,
yenye mapya na si huu wendawazimu wa siku zetu. Maana waingereza husema
“insanity is doing the same thing over and over again and expecting
different results.” Tuachane na wendawazimu huku tukijitofautisha na
mafisadi ili mataifa mengine yasiendelee kutucheka kwa kuruhusu taifa
letu kuwa shamba la bibi tena bibi mwenyewe hamnazo. Imetosha, wananchi
wanapaswa kuanza kwajibika kwa kuwawajibishwa watawala fisadi na wachovu
na wabovu.
Chanzo: Tanzania Daima leo.