Monday, November 24, 2014

Serikali yapiga mnada madini


chin
 
Arusha. Serikali imeuza kwa mnada aina mbalimbali ya madini yenye thamani ya zaidi ya Sh100 milioni yaliyokamatwa wakati yakitoroshwa nje ya nchi.
Mnada huo uliendeshwa jana na mwenyekiti wa bodi ya ushauri wa madini, Richard Kasesela akisaidiana na maofisa wa Wakala wa Ukaguzi wa Madini (TMAA), wakati wa maonyesho ya kimataifa ya madini yanayoendelea jijini Arusha.
Meneja uthamini wa madini kutoka TMAA, George Kaseza alisema madini yaliyopigwa mnada yalikamatwa kwenye vituo mbalimbali vya ukaguzi, vikiwamo viwanja vya ndege na maeneo ya mipakani.
“Madini haya yalikamatwa yakisafirishwa bila vibali maalumu vinavyoruhusu yakauzwe nje ya nchi wala kulipiwa ushuru na kodi ya Serikali,” alisema Kasesela.
Alisema Serikali imefikia hatua ya kupiga mnada madini hayo baada ya kuyataifisha kutokana na amri ya mahakama baada ya watuhumiwa waliokamatwa wakisafirisha nje ya nchi kutiwa hatiani na baadhi kuhukumiwa vifungo au faini.
Naibu katibu mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Ngozi Mwihava alisema miongoni mwa madini maarufu yaliyopigwa mnada ni dhahabu kilo moja na tanzanite ambayo hakutaja kiasi chake.
Serikali kuanza kukamata madini yanayosafirishwa nje ya nchi kimagendo imekuja baada ya kuweka ofisi za udhibiti wa madini katika viwanja vikubwa vya ndege vya Kilimanjaro, Mwanza na Dar es Salaam.
Kutoroshwa kwa madini hayo kwa njia mbalimbali, kumeifanya Kenya na India kuongoza duniani kwa kuuza madini ya tanzanite.

No comments:

Post a Comment