Monday, November 24, 2014

MAONI: Tumejiandaa vipi Uchaguzi Serikali za Mitaa?


 
 Baada ya kigugumizi cha muda mrefu, Serikali juzi ilitangaza kwamba uandikishaji wa wananchi kwa ajili ya kupiga kura katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utachukua siku saba, kuanzia Jumapili ijayo hadi Novemba 29, mwaka huu. Uchaguzi huo sasa umepangwa kufanyika Desemba 14 baada ya kuwapo mkanganyiko miongoni mwa viongozi wakuu serikalini, kwa kila mmoja kuibuka na ratiba ya kufikirika.
Wananchi wengi walikwazwa na hali hiyo, kwani wakati baadhi ya viongozi walisema uchaguzi huo ungeahirishwa hadi mapema mwakani, wengine walisema ungefanyika pamoja na Uchaguzi Mkuu mwishoni mwa mwaka ujao.
Wananchi walikwazwa na mkanganyiko huo kutokana na ukweli kwamba Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni muhimu mno, pengine kuliko uchaguzi mkuu wa nchi yoyote, kwani ndiyo hasa hutoa sura na taswira ya mamlaka ya wananchi walio wengi kuanzia ngazi za chini ambako ndiko viongozi katika ngazi zote nchini hupata uhalali wa kuongoza. Kwa maana hiyo, uchaguzi huo ni muhimu katika kudumisha demokrasia na utawala bora katika nchi. Ndiyo maana serikali nyingi duniani huelekeza nguvu na rasilimali nyingi katika kuhakikisha kwamba uchaguzi wa serikali za mitaa unafanyika na unakuwa huru na haki. Licha ya gharama kubwa, uchaguzi huo huhitaji muda wa kutosha kuhamasisha wananchi wajitokeze kupiga kura siku ya uchaguzi ili kuunda serikali ambayo itashughulikia matatizo ya wananchi katika ngazi hiyo muhimu.
Pamoja na kutangaza tarehe za kujiandikisha na kupiga kura, Serikali haionekani kama imefanya maandalizi ya kutosha kufanikisha uchaguzi huo. Wananchi, wakiwamo viongozi wa vyama vya siasa, wanahoji kwa nini haujafanyika uhamasishaji wa kutosha kwa wananchi ili wajiandikishe na kushiriki kikamilifu kugombea nafasi za uongozi au kuwachagua viongozi wanaofaa kuwaongoza. Wanasema haitoshi kwa Serikali kutaja gharama za kuendesha uchaguzi huo, bila kuhakikisha kwamba wagombea na wananchi kwa jumla wanafahamu taratibu na kanuni za uchaguzi huo, ikiwa ni pamoja na vituo vya kujiandikisha, kupigia kura, wasimamizi, wajibu na nafasi ya mawakala wa vyama vya siasa na sifa za wagombea na wapigakura.
Ikiwa zimebakia siku saba tu kabla ya kuanza uandikishaji wa wapigakura, mazingira yaliyopo hivi sasa hayaonyeshi ujio wa tukio kubwa kama hilo. Hivyo uwezekano wa wananchi wengi kutojiandikisha kupiga kura ni mkubwa. Tungetarajia ‘habari ya mjini’ hivi sasa iwe ni uchaguzi huo, lakini kinyume chake mazungumzo nchi nzima yameelekezwa kwenye mambo mengine, ikiwa ni pamoja na suala la akaunti ya Tegeta Escrow.
Pamoja na Serikali kuchelewa kuchukua hatua stahiki na kuupa uchaguzi huo kipaumbele, tunadhani inaweza kutumia muda mfupi uliobaki kuelekeza nguvu na rasilimali zake katika kuhakikisha kwamba uchaguzi huo unafanyika kwa mafanikio makubwa, hasa kwa kuzingatia kwamba dhumuni la kuwapo Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi ambao ndio chimbuko la mamlaka yote katika nchi yetu.
Tunaishauri Serikali iondoe kasoro zinazolalamikiwa, ikiwa ni pamoja na mkanganyiko katika mwongozo na baadhi ya kanuni za uchaguzi huo. Vinginevyo uchaguzi huo utagubikwa na sintofahamu na kusababisha vurugu ambazo zingeweza kuepukwa. Ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha uchaguzi huo unakuwa huru na wa haki, kwani kufanya hivyo kutasimika misingi ya utawala bora katika ngazi mbalimbali, kuanzia serikali za mitaa.

chin

No comments:

Post a Comment