Saturday, January 3, 2015

Kuasi kwa afisa mwandamizi wa al-Shabaab kwachochea mjadala juu ya programu ya msamaha

Kuasi kwa mkuu wa zamani wa intelijensia wa al-Shabaab, Zakariya Ismail Ahmed Hersi, kumechochea mjadala juu ya mpango wa msamaha wa serikali ya Somalia na faida za kuwasamehe maafisa wa al-Shabaab wanaotaka kujiondoa kwenye kundi hilo.
Vikosi vya usalama vikiwapekuwa wananchi wakati wa operesheni dhidi ya al-Shabaab mjini Mogadishu tarehe 8 Disemba 2014. Al-Shabaab imekuwa ikilaumiwa kuhusika na mauaji kadhaa yaliyowalenga wanasiasa, raia waliorejea nyumbani na yeyote mwenye mahusiano na kampuni za kigeni au serikali. [Mohamed Abdiwahab/AFP]
Hersi, aliyejisalimisha kwa wanajeshi wa Somalia walioko kwenye mkoa wa Gedo tarehe 27 Disemba, alikuwa anatakiwa na serikali ya Marekani kwa dau la dola milioni 3. Aliiasi al-Shabaab akiwa na watu wake wachache siku kadhaa baada ya muda wa msamaha uliongezwa na Rais Hassan Sheikh Mohamud kukaribia kukamilika.
"Ninaweza kuthibitisha kwamba siku chache zilizopita Zakariya Ismail Ahmed Hersi alikuja kwenye mikono ya serikali [ya shirikisho] na sasa anashikiliwa na vyombo vya usalama mjini Mogadishu," msemaji wa serikali, Ridwan Haji Abdiweli aliiambia Sabahi siku ya Ijumaa (tarehe 2 Januari).
Abdiweli alisema hakujua ikiwa msamaha wa rais utaendelea kwa mwaka huu, lakini akasema tangazo juu ya suala hilo litatolewa baadaye.
Kujisalimisha kwa Hersi kunaipa serikali ya Somalia fursa ya kuongeza uwezo wake wa kujua kazi za ndani za kundi hilo la wanamgambo na kuwasaka wengine wanaotaka kujiondoa kwenye kundi hilo, wanasema wachunguzi wa masuala ya usalama.
Vile vile kunatoa fursa kwa serikali kujitathmini upya juu ya namna inavyowashughulikia wale walioachana na al-Shabaab, alisema kanali mstaafu wa jeshi, Ahmed Omar Ga'al, ambaye alihudumu kama naibu mkuu wa usalama wa taifa mkoani Gedo wakati wa utawala wa Mohamed Siad Barre.
Hersi aliondoka al-Shabaab miezi kadhaa iliyopita baada ya kugombana na kiongozi wa wakati huo wa al-Shabaab, Ahmed Abdi Godane, ambaye aliuawa kwenye mashambulizi ya anga yaliyofanywa na Marekani mwezi Septemba, lakini hakuweza kupata fursa ya kuja upande wa serikali, alisema Ga'al.


"Niliambiwa na jamaa zake kwamba mtu huyu alitaka kujisalimisha kabla, lakini alikuwa akiogopa kwa kuwa hakuwa akiiamini programu ya msamaha ya serikali," alisema.
Wakati rais alipotangaza kwamba serikali ingeliongeza muda wa msamaha kwa wale wanaojiengua na al-Shabaab, kungelikuwa na mpango wa kujipenyeza kwenye kundi hilo kama njia ya kukusanya taarifa za kiintelijensia na kuwapa wapiganaji taarifa juu ya namna ya kuondoka, alisema Ga'al.
Vyombo vya usalama vya Somalia vilipaswa kujua juu ya ugomvi wa Hersi na Godane na kumfikia kumpa nafasi ya kupatiwa msamaha, alisema.
Kuifanya programu hii ya msamaha kufanya kazi vyema huko mbeleni, serikali inapaswa kuwa na mikakati mitatu, alisema.
"Kwanza, itumie pesa kuwavutia watu wengi kujiondoa al-Shabaab. Pili, itumie fursa panapotokezea migogoro ya ndani ya kundi la adui na [wanachama] wanaotaka kujajusiana. Tatu, watu wenye uzalendo lazima wawekwe ndani ya adui ili waweze kuiokoa nchi."
Ga'al alisema kufuata hatua hizo kutarahisisha upatikanaji wa taarifa za kiintelijensia zenye maana na kuishinda al-Shabaab. "Ni kwa kuwa na taarifa ndipo unapokuwa na uwezo dhidi ya adui yako," alisema.
Mafunzo kutoka waliojisalimisha awali
Profesa Yahye Ali Ibrahim, rais wa Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Somalia, alisema serikali ya Somalia inapaswa kutekeleza ahadi yake ya kuwapokea wanamgambo walioasi al-Shabaab kwa mikono wazi.
"Vile ambavyo serikali inamtendea Zakariya na watu kama yeye kutaamua ikiwa viongozi wengine zaidi wa al-Shabaab na wapiganaji wao watajisalimisha au la," Ibrahim aliiambia Sabahi, akiongeza kwamba ikiwa viongozi wa al-Shabaab wanaojisalimisha serikalini wanatendewa vyema, mamia ya wapiganaji waliovunjwa moyo na kundi hilo watashajiishwa kufuata.
Kujisalimisha kwa kiongozi wa zamani wa al-Shabaab mkoani Puntland, Sheikh Mohamed Said "Atom" , mwezi Juni na kiongozi wa zamani wa Hizbul Islam, Sheikh Hassan Dahir Aweys, mwaka mmoja kabla ya hapo ni mifano ambayo lazima ifanywe kuwa kigezo, alisema.
"Kwa kadiri tulivyoona, Sheikh Atom na Hassan Dahir Aweys wamekuwa wakitendewa vyema na tunatarajia kwamba Zakariya atatendewa hivyo hivyo," alisema Ibrahim.
Ibrahim aliitolea wito serikali ya Somalia kuongeza muda wa msamaha ili kuwekeza kwenye kipindi hiki cha mitihani ambacho al-Shabaab inakipitia.
"Serikali inapaswa kuzingatia watu ambao wamejipanga [kuasi] na kuwapa muda zaidi," alisema. "Itakuwa vigumu kwa mtu kuondoka ndani ya kipindi cha mwezi mmoja au miwili kwa sababu kuna njia nyingi ambazo mtu anapaswa kuzipitia hadi mtu kuweza kuliacha kundi hilo."
Ibrahim pia aliitolea wito serikali ya Somalia kutumia viongozi wa koo kutafuta kuzungumza na watu wa koo zao ambao ni sehemu ya al-Shabaab na ambao wanataka kuliacha kundi hilo.
"Kwa mfano, Zakariya alisalimishakatika mkoa ambao ametoka ingawa angeweza kujisalimisha katika mkoa mwingine. Hii inaonyesha kwamba alikuwa na imani katika ukoo wake," alisema.
"Hata hivyo, serikali inapaswa kuwa mwangalifu kuhusu wale ambao wana nyuso mbili [kama mawakala upande huu na upande mwengine], wale ambao hujifanya wamejisalimisha wakiwa bado wanafanya kazi na al-Shabaab," profesa Ibrahim aliongeza. "Suala hilo lazima lifuatiliwe kwa makini."
Hakuna wasiwasi kwamba Hersi angepewa msamaha wa rais katika mtindo ule ule aliopewa Aweys na Atom kabla yake, alisema Ibrahim Berow Ibrahim, mwenye umri wa miaka 32, mkazi wa Mogadishu.
"Mtu huyu ni kama wao. Msamaha ulitolewa kwa mwanachama wowote walioasi kutoka kwa al-Shabaab na kujitokeza mbele kutumia fursa hiyo," Ibrahim alisema.
Yeye alitetea msamaha wa serikali ilioutoa kwa walioasi al-Shabaab, akisema hakuna tofauti na wababe wa vita waliofanya uhalifu mkubwa wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe na sasa wameweka chini silaha zao na hata kutumikia katika shirikisho na tawala za kikanda.
"Kwa zaidi ya miaka 20 Somalia ilikuwa katika vita, watu wengi walishiriki katika vita vile. Kama wababe wale wa vita wanashitakiwa, kwa hivyo Hersi na wengine kama yeye lazima washitakiwe pia," alisema, na kuongeza kwamba msamaha lazima kuheshimiwa ili nchi iweze kusonga mbele.
Haki haikwepeki
Lakini Badrudin Ahmed Egale, mwenye umri wa miaka 28 na mkazi wa Mogadishu, yeye ana mtazamo wa chini wa kusamehe. Alisema hakukuwa na sababu ya msamaha kwa viongozi wa al-Shabaab ambao wamesababisha uharibifu usiokadirika katika Somalia na Afrika Mashariki yote.
"Vipi inawezekana kumsamahe mtu ambaye aliua watu wote wale bila sababu? Je hilo halitasababisha mtu mwingine kufanya kitu fulani kesho na kusamahewa?" aliiambia Sabahi. "Watu hawa wanapaswa kuadhibiwa ili iwe hakuna mtu mwingine anayejaribu kuidhuru jamii hii."
Egale alisema kuwa kila mwananchi ni sawa mbele ya sheria na mtu yeyote anayetenda uhalifu lazima apelekwe mbele ya sheria na kupata adhabu anayostahiki.
"Mtu huyu hakutenda uhalifu dhidi ya rais au waziri, yeye aliwadhuru na kuwaua watoto wa baba na mama, yeye alifanya watoto mayatima na akawafanya wajane wanawake vijana ambao walikuwa ndio kwanza wanaanza maisha yao," Egale alisema. "Jinsi gani rais anaweza kumsamehe mtu kama huyo?"
"Zakariya kwa sasa anashikilia nafasi ya mkuu wa upelelezi au Amniyat, ambacho ni kitengo kikubwa zaidi cha al-Shabaab na ambacho kimeua watu wasio na hatia," alisema. Ninasema haki haiepukiki na Zakariya na wengine kama yeye lazima wapambane nayo."

No comments:

Post a Comment